Ayubu - Sura ya 16

1Ndipo Ayubu akajibu, na kusema,
2Nimesikia maneno mengi mfano wa hayo; Ninyi nyote ni wafariji wenye kutaabisha.
3Je! Maneno yasiyo faida yatakuwa na mwisho? Au, kuna nini kinachokukasirisha, hata ukajibu?
4Mimi nami ningeweza kunena kama ninyi; Kama roho zenu zingekuwa mahali pa roho yangu, Ningeweza kutunga maneno juu yenu, Na kuwatikisia ninyi kichwa changu.
5Lakini ningewatia nguvu kwa kinywa changu, Na utuzo wa midomo yangu ungetuliza.
6Nijapokuwa nanena, huzuni yangu haitulizwi; Nijapokuwa najizuia, nimepunguziwa kitu gani?
7Lakini sasa amenichokesha; Jamii yangu yote umeifanya ukiwa.
8Umenishika sana, ni ushahidi juu yangu; Na kukonda kwangu kwaniinukia, kwanishuhudia usoni pangu.
9Amenirarua katika ghadhabu zake, na kunionea; Amesaga-saga meno juu yangu; Mtesi wangu hunikazia macho makali.
10Wamenifumbulia vinywa vyao; Wamenipiga shavuni kwa kunitukana; Hujikutanisha pamoja juu yangu.
11Mungu amenitia kwa hao wapotovu, Na kunitupa mikononi mwao waovu.
12Nilikuwa katika raha, naye akanivunja-vunja; Naam, amenishika shingo, na kuniponda; Tena amenisimamisha niwe shabaha yake.
13Wapigaji wake wa mishale hunizingira kotekote, Hunipasua viuno vyangu, asinihurumie; Nyonga zangu amezimwaga juu ya nchi.
14Hunivunja kwa uvunjifu juu ya uvunjifu; Hunishambulia mfano wa jitu shujaa.
15Nimeshona nguo ya magunia juu ya mwili wangu, Na pembe yangu nimeidhili uvumbini.
16Uso wangu umeharibika kwa kutoa machozi, Na giza tupu li katika kope zangu;
17Ijapokuwa hapana jeuri mikononi mwangu, Na kuomba kwangu ni safi.
18Ee nchi, usiifunike damu yangu, Na kilio changu kisipate mahali pa kupumzika.
19Hata sasa, tazama, shahidi wangu yuko mbinguni. Na huyo atakayenidhamini yuko juu.
20Rafiki zangu hunidharau; Lakini jicho langu humwagia Mungu machozi;
21Laiti angemtolea mtu hoja mbele ya Mungu, Amtetee na mwanadamu mbele ya jirani yake.
22Kwani ikiisha pita miaka michache, Nitakwenda njia hiyo ambayo sitarudi tena.