Maombolezo - Sura ya 3

1Mimi ni mtu aliyeona mateso Kwa fimbo ya ghadhabu yake.
2Ameniongoza na kuniendesha katika giza Wala si katika nuru.
3Hakika juu yangu augeuza mkono wake Mara kwa mara mchana wote.
4Amechakaza nyama yangu na ngozi yangu; Ameivunja mifupa yangu.
5Amejenga boma juu yangu, Na kunizungusha uchungu na uchovu.
6Amenikalisha penye giza, Kama watu waliokufa zamani.
7Amenizinga pande zote hata siwezi kutoka; Ameufanya mnyororo wangu mzito.
8Naam, nikilia na kuomba msaada, Huyapinga maombi yangu.
9Ameziziba njia zangu kwa mawe yaliyochongwa; Ameyapotosha mapito yangu.
10Alivyo kwangu ni kama dubu aoteaye, Kama simba aliye mafichoni.
11Amezigeuza njia zangu, na kunirarua-rarua; Amenifanya ukiwa.
12Ameupinda upinde wake, Na kunifanya niwe shabaha kwa mshale.
13Amenichoma viuno Kwa mishale ya podo lake.
14Nimekuwa dhihaka kwa watu wangu wote; Wimbo wao mchana kutwa.
15Amenijaza uchungu, Amenikinaisha kwa pakanga.
16Amenivunja meno kwa changarawe; Amenifunika majivu.
17Umeniweka nafsi yangu mbali na amani; Nikasahau kufanikiwa.
18Nikasema, Nguvu zangu zimepotea, Na tumaini langu kwa Bwana.
19Kumbuka mateso yangu, na msiba wangu, Pakanga na nyongo.
20Nafsi yangu ikali ikiyakumbuka hayo, Nayo imeinama ndani yangu.
21Najikumbusha neno hili, Kwa hiyo nina matumaini.
22Ni huruma za Bwana kwamba hatuangamii, Kwa kuwa rehema zake hazikomi.
23Ni mpya kila siku asubuhi; Uaminifu wako ni mkuu.
24Bwana ndiye fungu langu, husema nafsi yangu, Kwa hiyo nitamtumaini yeye.
25Bwana ni mwema kwa hao wamngojeao, Kwa hiyo nafsi imtafutayo.
26Ni vema mtu autarajie wokovu wa Bwana Na kumngojea kwa utulivu.
27Ni vema mwanadamu aichukue nira Wakati wa ujana wake.
28Na akae peke yake na kunyamaza kimya; Kwa sababu Bwana ameweka hayo juu yake.
29Na atie kinywa chake mavumbini; Ikiwa yamkini liko tumaini.
30Na amwelekezee yule ampigaye shavu lake; Ashibishwe mashutumu.
31Kwa kuwa Bwana hatamtupa mtu Hata milele.
32Maana ajapomhuzunisha atamrehemu, Kwa kadiri ya wingi wa huruma zake.
33Maana moyo wake hapendi kuwatesa wanadamu. Wala kuwahuzunisha.
34Kuwaseta chini kwa miguu Wafungwa wote wa duniani,
35Kuipotosha hukumu ya mtu Mbele zake Aliye juu,
36Na kumnyima mtu haki yake, Hayo Bwana hayaridhii kabisa.
37Ni nani asemaye neno nalo likafanyika, Ikiwa Bwana hakuliagiza?
38Je! Katika kinywa chake Aliye juu Hayatoki maovu na mema?
39Mbona anung'unika mwanadamu aliye hai Mtu akiadhibiwa kwa dhambi zake?
40Na tuchunguze njia zetu na kuzijaribu, Na kumrudia Bwana tena.
41Na tumwinulie Mungu aliye mbinguni Mioyo yetu na mikono.
42Sisi tumekosa na kuasi; Wewe hukusamehe.
43Umetufunika kwa hasira na kutufuatia; Umeua, wala hukuona huruma.
44Umejifunika nafsi yako kwa wingu, Maombi yetu yasipite.
45Umetufanya kuwa takataka, na vifusi Katikati ya mataifa.
46Juu yetu adui zetu wote Wametupanulia vinywa vyao.
47Hofu imetujilia na shimo, Ukiwa na uharibifu.
48Jicho langu lachuruzika mito ya maji Kwa ajili ya uvunjifu wa binti ya watu wangu.
49Jicho langu latoka machozi lisikome, Wala haliachi;
50Hata Bwana atakapoangalia Na kutazama toka mbinguni.
51Jicho langu lanitia huzuni nafsini mwangu, Kwa sababu ya binti zote za mji wangu.
52Walio adui zangu bila sababu Wameniwinda sana kama ndege;
53Wameukatilia mbali uhai wangu gerezani, Na kutupa jiwe juu yangu.
54Maji mengi yalipita juu ya kichwa changu, Nikasema, Nimekatiliwa mbali.
55Naliliitia jina lako, Bwana, kutoka lile shimo Liendalo chini kabisa.
56Ukaisikia sauti yangu; usifiche sikio lako Ili usisikie pumzi yangu, kwa kilio changu.
57Ulinikaribia siku ile nilipokulilia; Ukasema, Usiogope.
58Ee Bwana umenitetea mateto ya nafsi yangu; Umeukomboa uhai wangu.
59Umekuona kudhulumiwa kwangu, Ee Bwana; Unihukumie neno langu.
60Umekiona kisasi chao chote, Na mashauri yao yote juu yangu.
61Ee Bwana, umeyasikia matukano yao, Na mashauri yao yote juu yangu;
62Midomo yao walioinuka juu yangu Na maazimio yao juu yangu mchana kutwa.
63Uangalie kuketi kwao, na kuinuka kwao; Wimbo wao ndio mimi.
64Utawalipa malipo, Ee Bwana, Sawasawa na kazi ya mikono yao.
65Utawapa ushupavu wa moyo; Laana yako juu yao.
66Utawafuatia kwa hasira, na kuwaangamiza Wasiwe tena chini ya mbingu za Bwana.