Hesabu - Sura ya 21

1Na Mkanaani, mfalme wa Aradi, aliyeketi upande wa Negebu, alisikia habari ya kuwa Israeli alikuja kwa njia ya Atharimu; basi akapigana na Israeli, na watu kadha wa kadha miongoni mwao akawateka mateka.
2Basi Israeli akaweka nadhiri kwa Bwana akasema, Kama wewe utawatia watu hawa mikononi mwangu kweli ndipo mimi nitaiharibu miji yao kabisa.
3Bwana akasikiza sauti ya Israeli, akawatia Wakanaani mikononi mwao; nao wakawaharibu wao na miji yao kabisa; na jina la mahali hapo likaitwa Horma.
4Wakasafiri kutoka mlima wa Hori kwa njia ya Bahari ya Shamu; ili kuizunguka nchi ya Edomu, watu wakafa moyo kwa sababu ya ile njia.
5Watu wakamnung'unikia Mungu, na Musa, Mbona mmetupandisha huku kutoka nchi ya Misri, ili tufe jangwani? Maana hapana chakula, wala hapana maji, na roho zetu zinakinai chakula hiki dhaifu.
6Bwana akatuma nyoka za moto kati ya watu, wakawauma, watu wengi wakafa.
7Watu wakamwendea Musa, wakasema, Tumefanya dhambi kwa sababu tumemnung'unikia Mungu, na wewe; utuombee kwa Bwana, atuondolee nyoka hawa. Basi Musa akawaombea watu.
8Bwana akamwambia Musa, Jifanyie nyoka ya shaba, ukaiweke juu ya mti, na itakuwa kila mtu aliyeumwa, aitazamapo ataishi.
9Musa akafanya nyoka ya shaba, akaiweka juu ya mti, hata ikiwa nyoka amemwuma mtu, alipoitazama ile nyoka ya shaba, akaishi.
10Kisha wana wa Israeli wakasafiri, wakapanga marago Obothi.
11Wakasafiri kutoka Obothi, wakapanga Iye-abarimu, katika jangwa iliyoelekea Moabu, upande wa maawio ya jua.
12Kutoka huko wakasafiri, wakapanga katika bonde la Zeredi.
13Kutoka huko wakasafiri, wakapanga upande wa pili wa Arnoni, ulio jangwani, utokao katika mpaka wa Waamori; maana, Arnoni ndio mpaka wa Moabu, kati ya Moabu na Waamori.
14Kwa hiyo imesemwa katika chuo cha Vita vya Bwana, Wahebu katika Sufa, Na bonde za Arnoni,
15Na matelemko ya hizo bonde Kwenye kutelemkia maskani ya Ari, Na kutegemea mpaka wa Moabu.
16Kutoka huko wakasafiri kwenda Beeri; ni kisima ambacho Bwana alimwambia Musa, Uwakutanishe watu, nami nitawapa maji.
17Ndipo Israeli wakaimba wimbo huu; Bubujika Ee kisima; kiimbieni;
18Kisima walichokichimba wakuu, Ambacho wakuu wa watu wakakifukua, Kwa fimbo za enzi, kwa fimbo zao.
19na kutoka Matana wakaenda Nahalieli; na kutoka Nahalieli wakaenda Bamothi;
20na kutoka Bamothi wakaenda bondeni kwenye konde la Moabu, hata kilele cha Pisga, kielekeacho chini jangwani.
21Kisha Israeli akatuma wajumbe kumwendea Sihoni mfalme wa Waamori, na kusema,
22Nipe ruhusa nipite katika nchi yako; hatutageuka kando kwenda mashambani, wala kuingia katika mashamba ya mizabibu hatutakunywa maji ya visimani; tutakwenda kwa njia kuu ya mfalme, hata tutakapokuwa tumepita mpaka wako.
23Lakini Sihoni hakukubali kumwacha Israeli kupita katika mpaka wake; bali Sihoni akawakutanisha watu wake wote, akatoka aende kupigana na Israeli jangwani, akafika mpaka Yahasa; akapigana na Israeli.
24Israeli wakampiga kwa makali ya upanga, na kuimiliki nchi yake, tangu mto wa Arnoni hata mto wa Yaboki, mpaka nchi ya wana wa Amoni; kwa kuwa mpaka wa wana wa Amoni ulikuwa una nguvu.
25Basi Israeli wakaitwaa miji hiyo yote; Israeli wakakaa katika miji yote ya Waamori, katika Heshboni, na miji yake yote.
26Kwa kuwa Heshboni ulikuwa ni mji wa Sihoni mfalme wa Waamori, aliyekuwa akipigana na mfalme wa Moabu wa mbele, na kumpokonya nchi yake yote mkononi mwake, mpaka mto wa Arnoni.
27Kwa hiyo, hao wanenao kwa mithali wasema, Njoni Heshboni, Mji wa Sihoni na ujengwe na kuthibitishwa;
28Maana, moto umetoka Heshboni, Umekuwa Ari ya Moabu, Mwali wa moto umetoka mji wa Sihoni; Wakuu wa mahali palipoinuka Arnoni
29Ole wako Moabu! Umeangamia, enyi watu wa Kemoshi; Amewatoa wanawe kuwa wakimbizi, Na binti zake waende utumwani, Wamwendee Sihoni mfalme wa Waamori.
30Tumewapigia mishale; Heshboni umepotea mpaka Diboni, Nasi tumeharibu mpaka Nofa, Ifikiliayo Medeba.
31Basi hivyo Israeli akaketi katika nchi ya Waamori.
32Kisha Musa akapeleka watu ili kupeleleza Yazeri, nao wakaitwaa miji yake, wakawafukuza Waamori waliokuwamo.
33Kisha wakageuka na kukwea kwa njia ya Bashani; na Ogu mfalme wa Bashani akaondoka apigane nao huko Edrei, yeye na watu wake wote.
34Bwana akamwambia Musa, Usimche; kwa kuwa nimekwisha mtia mkononi mwako, na watu wake wote, na nchi yake; nawe utamtenda kama ulivyomtenda Sihoni mfalme wa Waamori, aliyeketi Heshboni.
35Basi wakampiga, na wanawe, na watu wake wote, hata wasisaze kwake mtu ye yote; nao wakaimiliki nchi yake.