Hesabu - Sura ya 34

Hesabu - Sura ya 34

1Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia,

2Waagize wana wa Israeli, uwaambie, Mtakapoingia nchi ya Kanaani, (hii ndiyo nchi itakayowaangukia kuwa urithi, maana, hiyo nchi ya Kanaani kama mipaka yake ilivyo,)

3ndipo upande wenu wa kusini utakuwa tangu bara ya Sini kupita kando ya Edomu, na mpaka wenu wa kusini utakuwa tangu mwisho wa Bahari ya Chumvi kuelekea mashariki;

4kisha mpaka wenu utageuka kwenda upande wa kusini wa kukwelea kwake Akrabimu, kisha kupita kwendelea Sini; na kutokea kwake kutakuwa kuelekea upande wa kusini wa Kadesh-barnea; kisha utaendelea mpaka Hasar-adari, na kufikilia Azmoni;

5kisha mpaka utageuka kutoka Azmoni kwendelea kijito cha Misri, na kutokea kwake kutakuwa hapo baharini.

6Kisha mpaka wenu wa upande wa magharibi mtakuwa na bahari kubwa na mpaka wake; hii ndiyo mpaka wenu upande wa magharibi.

7Kisha mpaka wenu wa upande wa kaskazini utakuwa ni huu; kutoka bahari kubwa mtajiandikia mlima wa Hori;

8na kutoka mlima wa Hori mtaandika mpaka kuingilia kwake Hamathi; na kutokea kwake mpaka kutakuwa hapo Sedada;

9tena mpaka utatokea hata Zifroni, na kutokea kwake kutakuwa hapo Hasarenani; huo ndio mpaka wenu wa upande wa kaskazini.

10Kisha mtaandika mpaka wenu wa upande wa mashariki kutoka Hasarenani hata Shefamu;

11kisha mpaka utatelemka kutoka Shefamu mpaka Ribla, upande wa mashariki wa Aini; kisha mpaka utatelemka na kufikilia upande wa bahari ya Kinerethi upande wa mashariki;

12kisha mpaka utatelemkia Yordani, na kutokea kwake kutakuwa hapo katika Bahari ya Chumvi; hii ndiyo nchi yenu kama mipaka yake ilivyo kuizunguka pande zote.

13Kisha Musa akawaagiza wana wa Israeli, akisema, Hii ndiyo nchi mtakayoirithi kwa kupiga kura, ambayo Bwana ameagiza wapewe watu wa zile kabila kenda, na nusu ya kabila;

14kwa kuwa kabila ya wana wa Reubeni kwa nyumba za baba zao, na kabila ya wana wa Gadi kwa nyumba za baba zao, wamekwisha pata, na hiyo nusu ya kabila ya Manase wamekwisha pata urithi wao;

15hizo kabila mbili na nusu ya kabila wamekwisha pata urithi wao huko ng'ambo ya pili ya Yordani, hapo Yeriko, upande wa mashariki, kuelekea maawio ya jua.

16Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia,

17Haya ndiyo majina ya watu watakaowagawanyia nchi iwe urithi wenu; Eleazari kuhani, na Yoshua mwana wa Nuni.

18Kisha mtamtwaa mkuu mmoja wa kila kabila, ili waigawanye nchi iwe urithi wenu.

19Na majina ya watu hao ni haya; katika kabila ya Yuda, ni Kalebu mwana wa Yefune.

20Na katika kabila ya wana wa Simeoni, Shemueli mwana wa Amihudi.

21Katika kabila ya Benyamini, ni Elidadi mwana wa Kisloni.

22Na katika kabila ya wana wa Dani, mkuu, Buki mwana wa Yogli.

23Katika wana wa Yusufu; katika kabila ya wana wa Manase, mkuu, Hanieli mwana wa Efodi;

24na katika kabila ya wana wa Efraimu, mkuu, Kemueli mwana wa Shiftani.

25Na katika kabila ya wana wa Zabuloni, mkuu, Elisafani mwana wa Parnaki.

26Na katika kabila ya wana wa Isakari, mkuu, Paltieli mwana wa Azani.

27Na katika kabila ya wana wa Asheri, mkuu, Ahihudi mwana wa Shelomi.

28Na katika kabila ya wana wa Naftali, mkuu, Pedaheli mwana wa Amihudi.

29Hao ndio Bwana aliowaagiza wawagawanyie urithi wana wa Israeli katika nchi ya Kanaani.