Mithali - Sura ya 14

1Kila mwanamke aliye na hekima hujenga nyumba yake; Bali aliye mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe.
2Yeye aendaye kwa unyofu wake humcha Bwana; Bali aliye mkaidi katika njia zake humdharau.
3Katika kinywa cha mpumbavu mna fimbo ya kiburi, Bali midomo ya wenye hekima huwahifadhi.
4Zizi ni safi ambapo hapana ng'ombe; Bali nguvu za ng'ombe zaleta faida nyingi.
5Shahidi mwaminifu hatasema uongo; Bali shahidi wa uongo, pumzi zake ni uongo.
6Mwenye dharau hutafuta hekima, asiipate; Bali maarifa huwa mepesi kwa mwenye ufahamu.
7Toka mbele ya uso wa mpumbavu, Maana hutaona kwake midomo ya maarifa.
8Akili za mwenye busara ni kujua njia yake; Lakini upumbavu wa wapumbavu ni udanganyifu.
9Wapumbavu huidharau hatia; Bali upo upendeleo kwa wenye haki.
10Moyo huujua uchungu wa nafsi yake, Wala mgeni haishiriki furaha yake.
11Nyumba ya mtu mbaya itabomolewa; Bali hema ya mwenye haki itafanikiwa.
12Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu, Lakini mwisho wake ni njia za mauti.
13Hata wakati wa kucheka moyo huwa na huzuni; Na mwisho wa furaha ni uzito wa moyo.
14Ageukaye moyoni hushiba njia zake mwenyewe; Na mtu mwema ataridhika nafsini mwake.
15Mjinga huamini kila neno; Bali mwenye busara huangalia sana aendavyo.
16Mwenye hekima huogopa, akajitenga na uovu; Bali mpumbavu ana ufidhuli, na kujitumai.
17Yeye aonaye hasira upesi atatenda kwa ujinga; Na mtu mwenye hila mbaya huzirwa.
18Wajinga hurithi upumbavu; Bali wenye busara huvikwa taji ya maarifa.
19Wabaya huinama mbele ya wema, Na wasio haki malangoni mwao wenye haki.
20Maskini huchukiwa hata na jirani yake; Bali tajiri ana rafiki wengi.
21Amdharauye mwenzake afanya dhambi; Bali amhurumiaye maskini ana heri.
22Je! Hawakosi wawazao mabaya? Bali fadhili na kweli zina wao wawazao mema.
23Katika kila kazi mna faida; Bali maneno ya midomo huleta hasara tu.
24Taji ya wenye hekima ni mali zao; Bali upumbavu wa wajinga ni upumbavu tu.
25Shahidi wa kweli huponya nafsi za watu; Bali atoaye uongo hudanganya.
26Kumcha Bwana ni tumaini imara; Watoto wake watakuwa na kimbilio.
27Kumcha Bwana ni chemchemi ya uzima, Ili kuepukana na tanzi za mauti.
28Utukufu wa mfalme ni wingi wa watu wake; Bali uchache wa watu ni uharibifu wa mkuu wao.
29Asiye mwepesi wa hasira ana fahamu nyingi; Bali mwenye roho ya hamaki hutukuza upumbavu.
30Moyo ulio mzima ni uhai wa mwili; Bali husuda ni ubovu wa mifupa.
31Amwoneaye maskini humsuta Muumba wake; Bali yeye awahurumiaye wahitaji humheshimu.
32Mtu mbaya husukumwa chini katika kutenda mabaya kwake; Bali mwenye haki ana matumaini katika kufa kwake.
33Hekima hukaa katika moyo wake mwenye ufahamu; Bali yaliyo ndani ya wapumbavu hudhihirika.
34Haki huinua taifa; Bali dhambi ni aibu ya watu wo wote.
35Upendeleo wa mfalme humwelekea mtumwa atendaye kwa busara; Bali ghadhabu yake itakuwa juu yake aletaye aibu.