Mithali - Sura ya 15
1Jawabu la upole hugeuza hasira; Bali neno liumizalo huchochea ghadhabu.
2Ulimi wa mwenye hekima hutamka maarifa vizuri; Bali vinywa vya wapumbavu humwaga upumbavu.
3Macho ya Bwana yako kila mahali; Yakimchunguza mbaya na mwema.
4Ulimi safi ni mti wa uzima; Bali ukorofi wa ulimi huvunja moyo.
5Mpumbavu hudharau kurudiwa na babaye; Bali yeye aangaliaye maonyo hupata busara.
6Katika nyumba ya mwenye haki mna akiba nyingi; Bali mapato ya mtu mbaya huwa taabu tu.
7Midomo ya mwenye haki hueneza maarifa; Bali moyo wa mpumbavu haufanyi hivyo.
8Sadaka ya mtu mbaya ni chukizo kwa Bwana; Bali maombi ya mtu mnyofu ni furaha yake.
9Njia ya mtu mbaya ni chukizo kwa Bwana; Bali humpenda mtu afuatiaye wema.
10Adhabu kali ina yeye aiachaye njia; Naye achukiaye kukemewa atakufa.
11Kuzimu na Uharibifu vi wazi mbele za Bwana; Si zaidi basi, mioyo ya wanadamu?
12Mwenye mzaha hapendi kukaripiwa; Wala yeye hawaendei wenye hekima.
13Moyo wa furaha huchangamsha uso; Bali kwa huzuni ya moyo roho hupondeka.
14Moyo wa mwenye ufahamu hutafuta maarifa; Bali kinywa cha wapumbavu hula upumbavu.
15Siku zote za mtu ateswaye ni mbaya; Bali ukunjufu wa moyo ni karamu ya daima.
16Kuwa na mali chache pamoja na kumcha Bwana; Ni bora kuliko mali nyingi pamoja na taabu.
17Chakula cha mboga penye mapendano; Ni bora kuliko ng'ombe aliyenona pamoja na kuchukiana.
18Mtu wa hasira huchochea ugomvi; Bali asiye mwepesi wa hasira hutuliza mashindano.
19Njia ya mtu mvivu ni kama boma la miiba; Bali mapito yao wenye unyofu hufanyika njia kuu.
20Mwana mwenye hekima humfurahisha babaye; Bali mpumbavu humdharau mamaye.
21Upumbavu ni furaha kwake aliyepungukiwa na akili; Bali mwenye ufahamu huunyosha mwenendo wake.
22Pasipo mashauri makusudi hubatilika; Bali kwa wingi wa washauri huthibithika.
23Mtu hulifurahia jibu la kinywa chake; Na neno linenwalo wakati wa kufaa ni jema kama nini!
24Kwa mtu mwenye akili njia ya uhai huenda juu; Ili atoke katika kuzimu chini.
25Bwana ataing'oa nyumba ya mwenye kiburi; Bali atauthibitisha mpaka wa mjane.
26Mashauri mabaya ni chukizo kwa Bwana; Bali maneno yapendezayo ni safi.
27Atamaniye faida huifadhaisha nyumba yake mwenyewe; Bali achukiaye zawadi ataishi.
28Moyo wa mwenye haki hufikiri jinsi atakavyojibu; Bali kinywa cha wasio haki humwaga mabaya.
29Bwana yu mbali na wasio haki; Bali huisikia sala ya mwenye haki.
30Mng'ao wa macho huufurahisha moyo; Habari njema huinenepesha mifupa.
31Sikio lisikilizalo lawama yenye uhai Litakaa kati yao wenye hekima.
32Akataaye maonyo huidharau nafsi yake mwenyewe; Bali yeye asikilizaye lawama hujipatia ufahamu.
33Kumcha Bwana ni maonyo ya hekima; Na kabla ya heshima hutangulia unyenyekevu.

Swahili
Italiano (it-IT)
Português do Brasil (pt-BR)
Polski (PL)
Deutsch (Deutschland)
Français (France)
Español (España)
Українська Біблія у перекладі Огієнка
English Bible - 21ST CENTURY KING JAMES (KJ21)