Mithali - Sura ya 29

Mithali - Sura ya 29

1Aonywaye mara nyingi akishupaza shingo, Atavunjika ghafula, wala hapati dawa.

2Wenye haki wakiwa na amri, watu hufurahi; Bali mwovu atawalapo, watu huugua.

3Apendaye hekima humfurahisha babaye; Bali ashikamanaye na makahaba hutapanya mali.

4Mfalme huithibitisha nchi kwa hukumu; Bali yeye apokeaye rushwa huipindua.

5Mwenye kujipendekeza kwa jirani yake, Hutandika wavu ili kuitega miguu yake.

6Kuna mtego katika kosa la mtu mbaya; Bali mwenye haki huimba na kufurahi.

7Mwenye haki huyaangalia madai ya maskini; Bali mtu mbaya hana ufahamu hata ayajue.

8Watu wenye dharau huwasha mji moto; Bali wenye hekima hugeuzia mbali ghadhabu.

9Mwenye hekima akijadiliana na mpumbavu; Akikasirika au akicheka, pia hapana raha.

10Wamwagao damu humchukia mtu mkamilifu; Bali wenye haki humtunza nafsi yake.

11Mpumbavu hudhihirisha hasira yake yote; Bali mwenye hekima huizuia na kuituliza.

12Mwenye kutawala akisikiliza uongo; Basi watumishi wake wote watakuwa waovu.

13Maskini na mdhalimu hukutana pamoja; Bwana huwatia nuru macho yao wote wawili.

14Mfalme awahukumuye maskini kwa uaminifu; Kiti chake cha enzi kitathibitika milele.

15Fimbo na maonyo hutia hekima; Bali mwana aliyeachiliwa humwaibisha mamaye.

16Waovu wakiongezeka, maasi huongezeka; Bali wenye haki watayatazama maanguko yao.

17Mrudi mwanao naye atakustarehesha; Naam, atakufurahisha nafsi yako.

18Pasipo maono, watu huacha kujizuia; Bali ana heri mtu yule aishikaye sheria.

19Haitoshi mtumwa kuonywa kwa maneno; Maana ajapoyafahamu hataitika.

20Je! Umemwona mtu mwenye kuhamaki katika maneno? Afadhali kumtumaini mpumbavu kuliko yeye.

21Amtunduiaye mtumwa wake tangu utoto, Mwisho wake atakuwa ni mwanawe.

22Mtu wa hasira huchochea ugomvi; Na mtu mwenye ghadhabu huasi sana.

23Kiburi cha mtu kitamshusha; Bali mwenye roho ya unyenyekevu ataheshimiwa.

24Mshiriki wa mwivi huichukia nafsi yake mwenyewe; Asikia maapizo, wala hana neno.

25Kuwaogopa wanadamu huleta mtego; Bali amtumainiye Bwana atakuwa salama.

26Watu wengi hutafuta upendeleo wa mkuu; Bali hukumu ya kila mtu hutoka kwa Bwana

27Mtu aliye dhalimu ni chukizo kwa wenye haki; Na mnyofu wa mwenendo ni chukizo kwa waovu.