Zaburi - Sura ya 106

Zaburi - Sura ya 106

1Haleluya. Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema, Kwa maana fadhili zake ni za milele.

2Nani awezaye kuyanena matendo makuu ya Bwana, Kuzihubiri sifa zake zote?

3Heri washikao hukumu, Na kutenda haki sikuzote.

4Ee Bwana, unikumbuke mimi, Kwa kibali uliyo nayo kwa watu wako. Unijilie kwa wokovu wako,

5Ili niuone wema wa wateule wako. Nipate kuifurahia furaha ya taifa lako, Na kujisifu pamoja na watu wako.

6Tumetenda dhambi pamoja na baba zetu, Tumetenda maovu, tumefanya ubaya.

7Baba zetu katika Misri Hawakufikiri matendo yako ya ajabu; Hawakukumbuka wingi wa fadhili zako; Wakaasi penye bahari, bahari ya Shamu.

8Lakini akawaokoa kwa ajili ya jina lake, Ayadhihirishe matendo yake makuu.

9Akaikemea bahari ya Shamu ikakauka, Akawaongoza vilindini kana kwamba ni uwanda.

10Akawaokoa na mkono wa mtu aliyewachukia, Na kuwakomboa na mkono wa adui zao.

11Maji yakawafunika watesi wao, Hakusalia hata mmoja wao.

12Ndipo walipoyaamini maneno yake, Waliziimba sifa zake.

13Wakayasahau matendo yake kwa haraka, Hawakulingojea shauri lake.

14Bali walitamani sana jangwani, Wakamjaribu Mungu nyikani.

15Akawapa walichomtaka, Akawakondesha roho zao.

16Wakamhusudu Musa matuoni, Na Haruni, mtakatifu wa Bwana.

17Nchi ikapasuka ikammeza Dathani, Ikaufunika mkutano wa Abiramu.

18Moto ukawaka katika mkutano wao, Miali yake ikawateketeza wabaya.

19Walifanya ndama huko Horebu, Wakaisujudia sanamu ya kuyeyuka.

20Wakaubadili utukufu wao Kuwa mfano wa ng'ombe mla majani.

21Wakamsahau Mungu, mwokozi wao, Aliyetenda makuu katika Misri.

22Matendo ya ajabu katika nchi ya Hamu, Mambo ya kutisha penye bahari ya Shamu.

23Akasema ya kuwa atawaangamiza Kama Musa, mteule wake, asingalisimama, Mbele zake kama mahali palipobomoka, Ili aigeuze hasira yake asije akawaharibu.

24Wakaidharau nchi ile ya kupendeza, Wala hawakuliamini neno lake.

25Bali wakanung'unika hemani mwao, Wala hawakuisikiliza sauti ya Bwana.

26Ndipo alipowainulia mkono wake, Ya kuwa atawaangamiza jangwani,

27Na kuwatawanya wazao wao kati ya mataifa, Na kuwatapanya katika nchi mbali.

28Wakajiambatiza na Baal-Peori, Wakazila dhabihu za wafu.

29Wakamkasirisha kwa matendo yao; Tauni ikawashambulia.

30Ndipo Finehasi akasimama akafanya hukumu; Tauni ikazuiliwa.

31Akahesabiwa kuwa ana haki Kizazi baada ya kizazi hata milele.

32Wakamghadhibisha penye maji ya Meriba, Hasara ikampata Musa kwa ajili yao,

33Kwa sababu waliiasi roho yake, Akasema yasiyofaa kwa midomo yake.

34Hawakuwaharibu watu wa nchi Kama Bwana alivyowaambia;

35Bali walijichanganya na mataifa, Wakajifunza matendo yao.

36Wakazitumikia sanamu zao, Nazo zikawa mtego kwao.

37Naam, walitoa wana wao na binti zao Kuwa dhabihu kwa mashetani.

38Wakamwaga damu isiyo na hatia, Damu ya wana wao na binti zao, Waliowatoa dhabihu kwa sanamu za Kanaani; Nchi ikatiwa unajisi kwa damu.

39Ndivyo walivyotiwa uchafu kwa kazi zao, Wakafanya uasherati kwa matendo yao.

40Hasira ya Bwana ikawaka juu ya watu wake, Akauchukia urithi wake.

41Akawatia mikononi mwa mataifa, Nao waliowachukia wakawatawala.

42Adui zao wakawaonea, Wakatiishwa chini ya mkono wao.

43Mara nyingi aliwaponya, Bali walikuwa wakimwasi kwa mashauri yao, Wakadhilika katika uovu wao.

44Lakini aliyaangalia mateso yao, Aliposikia kilio chao.

45Akawakumbukia agano lake; Akawahurumia kwa wingi wa fadhili zake;

46Akawajalia kuhurumiwa Na watu wote waliowateka.

47Ee Bwana, Mungu wetu, utuokoe, Utukusanye kwa kututoa katika mataifa, Tulishukuru jina lako takatifu, Tuzifanyie shangwe sifa zako.

48Na ahimidiwe Bwana, Mungu wa Israeli, Tangu milele hata milele. Watu wote na waseme, Amina. Haleluya.