Zaburi - Sura ya 108

Zaburi - Sura ya 108

1Ee Mungu, moyo wangu u thabiti, Nitaimba, nitaimba zaburi, Naam, kwa utukufu wangu.

2Amka, kinanda na kinubi, Nitaamka alfajiri.

3Ee Bwana, nitakushukuru kati ya watu, Nitakuimbia zaburi kati ya mataifa.

4Maana fadhili zako ni kubwa hata mbinguni, Na uaminifu wako hata mawinguni.

5Ee Mungu, utukuzwe juu ya mbingu, Na juu ya nchi yote uwe utukufu wako.

6Ili wapenzi wako waopolewe, Uokoe kwa mkono wako wa kuume, uniitikie.

7Mungu amenena kwa utakatifu wake, Nami nitashangilia. Nitaigawanya Shekemu, Nitalipima bonde la Sukothi.

8Gileadi ni yangu, na Manase ni yangu, Na Efraimu ni nguvu ya kichwa changu. Yuda ni fimbo yangu ya kifalme,

9Moabu ni bakuli langu la kunawia. Nitamtupia Edomu kiatu changu, Na kumpigia Filisti kelele za vita.

10Ni nani atakayenipeleka hata mji wenye boma? Ni nani atakayeniongoza hata Edomu?

11Ee Mungu, si Wewe uliyetutupa? Wala, Ee Mungu, hutoki na majeshi yetu?

12Utuletee msaada juu ya mtesi, Maana wokovu wa binadamu haufai.

13Kwa msaada wa Mungu tutatenda makuu, Maana Yeye atawakanyaga watesi wetu.