Zaburi - Sura ya 62

Zaburi - Sura ya 62

1Nafsi yangu yamngoja Mungu peke yake kwa kimya, Wokovu wangu hutoka kwake.

2Yeye tu ndiye mwamba wangu na wokovu wangu, Ngome yangu, sitatikisika sana.

3Hata lini mtamshambulia mtu, Mpate kumwua ninyi nyote pamoja? Kama ukuta unaoinama, Kama kitalu kilicho tayari kuanguka,

4Hufanya shauri kumwangusha tu katika cheo chake; Huufurahia uongo. Kwa kinywa chao hubariki; Kwa moyo wao hulaani.

5Nafsi yangu, umngoje Mungu peke yake kwa kimya. Tumaini langu hutoka kwake.

6Yeye tu ndiye mwamba wangu na wokovu wangu, Ngome yangu, sitatikisika sana.

7Kwa Mungu wokovu wangu, Na utukufu wangu; Mwamba wa nguvu zangu, Na kimbilio langu ni kwa Mungu.

8Enyi watu, mtumainini sikuzote, Ifunueni mioyo yenu mbele zake; Mungu ndiye kimbilio letu.

9Hakika binadamu ni ubatili, Na wenye cheo ni uongo, Katika mizani huinuka; Wote pamoja ni hafifu kuliko ubatili.

10Msiitumainie dhuluma, Wala msijivune kwa unyang'anyi; Mali izidipo msiiangalie sana moyoni.

11Mara moja amenena Mungu; Mara mbili nimeyasikia haya, Ya kuwa nguvu zina Mungu,

12Na fadhili ziko kwako, Ee Bwana; Maana ndiwe umlipaye kila mtu Sawasawa na haki yake.